UPADRISHO KIABAKARI: Shemasi Paul Bhega OFM apadrishwa.

08/07/2021

Askofu wa Jimbo Katoliki la Musoma amemtaka Padri mpya PAUL BHEGGA OFM wa shirika la ndugu wadogo wa Kapuchini kuhakikisha sehemu yoyote atakayopangiwa kufanya Utume wake, anayatunza mazingira kwa kuwa kuna uharibifu mkubwa sana wa mazingira ambao unasababisha mabadiliko ya hali ya hewa.

Akizungumza wakati wa Misa Takatifu ya Upadrisho uliofanyika katika Parokia ya Kiabakari Julai 8 mwaka huu, Askofu Msonganzila amesema ,kwa sasa kuna haja ya kuendelea kutoa elimu kwa waamini wetu juu ya umuhimu wa utunzaji wa mazingira .

“Naomba sana umfuate Mtakatifu Francisco aliyejua kutunza mazingira ,tunza mazingira ili yakutunze ,lakini pia kumbuka kuwa kipindi hiki watu hawamuogopi Mungu, jitahidi sana kujiweka karibu na Mungu ili uweze kuyashinda yote ikiwa ni pamoja na kujikinga na gonjwa hili la Corona”amesema Askofu Msonganzila.

Katika sherehe hizo Askofu amewaomba waamini kuendelea kuchukua tahadhali ya uwepo wa ugonjwa wa Corona na kuzingatia ushauri unaotolewa na wataalam pamoja na Wizara ya afya,hasa kuvaa barakoa na kutumia vitakasa mikono.



Na Veronica Modest, Musoma.